إِلَّا تَنصُرُوهُ فَقَدۡ نَصَرَهُ ٱللَّهُ إِذۡ أَخۡرَجَهُ ٱلَّذِينَ كَفَرُواْ ثَانِيَ ٱثۡنَيۡنِ إِذۡ هُمَا فِي ٱلۡغَارِ إِذۡ يَقُولُ لِصَٰحِبِهِۦ لَا تَحۡزَنۡ إِنَّ ٱللَّهَ مَعَنَاۖ فَأَنزَلَ ٱللَّهُ سَكِينَتَهُۥ عَلَيۡهِ وَأَيَّدَهُۥ بِجُنُودٖ لَّمۡ تَرَوۡهَا وَجَعَلَ كَلِمَةَ ٱلَّذِينَ كَفَرُواْ ٱلسُّفۡلَىٰۗ وَكَلِمَةُ ٱللَّهِ هِيَ ٱلۡعُلۡيَاۗ وَٱللَّهُ عَزِيزٌ حَكِيمٌ
Ikiwa nyinyi hamtamnusuru Mtume, basi Mwenyezi Mungu alikwisha mnusuru walipo mtoa walio kufuru, naye ni wa pili katika wawili walipo kuwa katika pango, naye akamwambia sahibu yake: Usihuzunike. Hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja nasi. Mwenyezi Mungu akamteremshia utulivu wake, na akamuunga mkono kwa majeshi msiyo yaona, na akalifanya neno la walio kufuru kuwa chini, na Neno la Mwenyezi Mungu kuwa ndilo juu. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye nguvu Mwenye hikima.
Ali Muhsin Al - Swahili translation
Enyi mkusanyiko wa Maswahaba wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema za Mwenyezi Mungu na amani zimshukiye, msipotoka pamoja na yeye anapowataka mtoke, na msipomtetea, basi Mwenyezi Mungu Alimsaidia na kumtetea siku ile Makafiri wa Kikureshi walipomtoa kwenye mji wake wa Maka, na yeye ni wapili kati ya wawili( yeye na Abu Bakr al-Siddiq, radhi ya Mwenyezi Mungu imshukiye) wakawafanya ibidi waingie pangoni katika jabali la Thawr, wakakaa humo siku tatu, pindi alipomwambia rafiki Yake Abu Bakr, alipomuona ameingiwa na kicho juu yake, «Usihuzunike, Mungu Yupo pamoja na sisi» kwa kutunusuru na kutupa nguvu. Hapo Mwenyezi Mungu Aliteremsha utulivu kwenye moyo wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani imshukiye, na akamsaidia kwa askari ambao hakuna aliowaona kati ya wanadamu, nao ni Malaika. Hapo Mwenyezi Mungu Alimuokoa na adui yake, Akawafanya wanyonge maadui wake, Akalifanya neno la waliokanusha ndilo la chini na neno la Mwenyezi Mungu ndilo la juu. Na hilo ni kwa kuliinua juu jambo la Uislamu. Na Mwenyezi Mungu ni Mshindi katika ufalme Wake, ni Mwingi wa hekima katika kuyaendesha mambo ya waja Wake. Katika aya hii pana kitambulisho cha cheo cha Abu Bakr, radhi ya Mwenyezi Mungu zimshukie.
الترجمة السواحلية - عبد الله محمد وناصر خميس