ترجمة سورة القلم

الترجمة السواحلية - عبد الله محمد وناصر خميس
ترجمة معاني سورة القلم باللغة السواحلية من كتاب الترجمة السواحلية - عبد الله محمد وناصر خميس .

«Nūn» Yametangulia maelezo kuhusu herufi zilizokatwakatwa na kutengwa mwanzo wa sura ya Al-Baqarah.
Anaapa Mwenyezi Mungu kwa Kalamu ambayo kwayo Malaika na watu wanaandikia, na kwa kile wanachokiandika cha kheri, manufaa na aina za elimu.
Hukuwa wewe, ewe Mtume, kwa sababu ya neema ya Mwenyezi Mungu kwako, ya unabii na utume, ni mchache wa akili wala mwenye uduni wa maoni. Na wewe una malipo makubwa yasiyopunguzwa wala kukatwa kwa yale matatizo unayopambana nayo ya ufikishaji ujumbe.
Na hakika wewe, ewe Mtume, uko juu ya tabia kubwa, nazo ni zile tabia njema zilizomo kwenye Qur’ani. Kwani kule kuifuata Qur’ani kulikuwa ni sifa yake, akitekeleza amri zake na kukomeka na yale yanayokatazwa nayo.
Kwa kipindi cha karibu kijacho, utaona ewe Mtume, na wataona
makafiri ugonjwa wa akili na wazimu viko kwa nani miongoni mwenu?
Hakika Mola wako , kutakasika ni Kwake, Ndiye Mjuzi zaidi wa kumjua mpotofu aliyeenda kombo na Dini ya Mwenyezi Mungu na njia ya uongofu, na Yeye Ndiye Mjuzi zaidi wa kumjua mchamungu aliyeongoka kwenye njia ya haki.
Basi jikite kwenye msimamo ulionao, ewe Mtume, wa kuenda kinyume na wakanushaji, na wala usiwatii.
Wanatamani na wanapenda lau wewe unakuwa laini kwao na kuwakubalia baadhi ya misimamo waliyonayo, na wao wakawa laini kwako.
Usimkubalie, ewe Mtume, kila mtu mweye kuapa mayamini sana,
mrongo sana, mtwevu, msengenyaji watu, anayetembea baina yao kwa kuchochea ugomvi na kuchukua maneno ya baadhi yao kuwapelekea wengine kwa lengo la kuharibu baina yao, bahili wa mali mwenye uchoyo wa kuyatumia katika njia ya haki,
mwenye kuzuia sana ufanyaji wema, anayevuka mpaka wake katika kuwafanyia watu uadui na kutumia yaliyohartamishwa, mwingi wa madhambi,
mshupavu katika ukafiri wake, mchafu na muovu na anayenasibishwa na baba asiye wake.
Na kwa kuwa yeye ni mwenye mali na wana ndipo akakiuka mipaka na akaifanyia kiburi haki.
Ikawa akisomewa aya za Qur’ani na mtu yoyote huzikanusha na kusema kuwa hizo ni maneno ya urongo na itikadi za watu waliopita. Aya hizi, ingawa zimeteremka kwa baadhi ya washirikina, kama vile al-Walīd bin \al-Mughīrah, zina onyo ndani yake kwa Muislamu asikubaliane na anayesifika kwa sifa hizi zenye kutukanika.
Tutaweka alama ya kudumu juu ya pua yake isiyomuepuka, ili afedheheke mbele za watu.
Sisi tumewatahini watu wa Makkah kwa njaa na ukame kama tulivyowatahini wenye shamba walipoapa wakiwa pamoja kwamba watakwenda kuvuna matunda ya shamba lao asubuhi mapema, ili wasiokuwa wao, kati ya masikini na mfano wao, wasipate kula katika mavuno hayo.
Na wasiseme walipopanga hayo, «Mwenyezi Mungu Akitaka».
Mwenyezi Mungu akaliteremshia shamba hilo moto ukaliteketeza kipindi cha usiku na hali wao wakiwa wamelala.
Na likapambaukiwa nalo lishachomeka limekuwa leusi kama usiku wa giza.
Hapo wakaitana kipindi cha asubuhi.
«Haya tokeni mapema mwende kwenye shamba lenu iwapo bado mnataka kuvuna matunda!»
Wakatoka kwa haraka, huku wakinong’ onezana,
«Leo msimpe nafasi masikini yoyote kuingia shamba lenu.»
Wakaenda kipindi cha mwanzo wa mchana kuelekea kwenye shamba lao wakiwa na lengo baya la kuwanyima masikini matunda ya shamba, wakiwa wana uwezo kamili wa kulitekeleza hilo kulingana na madai yao.
Walipolishuhudia shamba lao limechomeka walilikataa na wakasema, ‘Kwa hakika tumepotea njia ya kulifikia!» na walipojua kuwa hilo ndilo shamba lao walisema,
«Bali sisi tumekoseshwa mazao yake kwa sababu ya nia yetu ya uchoyo na kuwanyima masikini.»
Akasema muadilifu zaidi miongoni mwao, «Kwani sikuwaambia myafunge maneno yenu na matakwa ya mwenyezi Mungu kwa kusema ‘Mwenyezi Mungu Akitaka’?»
Hapo wakasema, baada ya kurudi kwenye fahamu za uongofu, «Mwenyezi Mungu Mola wetu Ametakasika na udhalimu katika haya yaliyotupata, lakini ni sisi ndio tuliojidhulumu nafsi zetu kwa kuacha kuyafunga maneno yetu na matakwa ya Mwenyezi Mungu na kwa lengo letu baya.»
Wakazungukiana wao kwa wao wakilaumiana kwa kuacha kuyafunga maneno yao na matakwa ya Mwenyezi Mungu na kwa lengo lao baya,
wakasema, «Ewe ole wetu! Sisi tulikuwa tumekiuka mpaka kwa kuwanyima masikini na kuenda kinyume na amri ya Mwenyezi Mungu.
Tunatarajia kwa Mola wetu kuwa Atatupa kilicho bora zaidi kuliko shamba letu, kwa kuwa tumetubia na tumekubali makosa yetu. Sisi tuna matumaini mema kwa Mola wetu, tunatarajia msamaha na tunaomba kheri. Mfano wa mateso hayo tuliyowatesa nayo wenye shamba ndivyo yanavyokuwa mateso yetu duniani kwa kila anayeenda kinyume na amri ya Mwenyezi Mungu na akazifanyia uchoyo neema za Mwenyezi Mungu Alizompa kwa kutotekeleza haki ya Mwenyezi Mungu katika neema hizo.
Na kwa hakika adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kubwa zaidi na ni kali zaidi kuliko adhabu ya duniani. Lau wao wangalijua wangalijiepusha na kila jambo lenye kusababisha kupata mateso hayo.
Hakika wale waliojikinga na mateso ya Mwenyezi Mungu kwa kufanya yale Aliyowaamrisha na kuacha yale Aliyoyakataza, watapata kwa Mola wao huko Akhera, mabustani ya Peponi ambayo ndani yake kuna starehe za daima.
Je tuwafanye wale wanaomnyenyekea Mwenyezi Mungu kwa kumtii ni kama wale waliokufuru?
Mna nini nyinyi? Vipi mnatoa uamuzi huu wa kudhalimu, mkalinganisha baina yao katika malipo?
Au nyinyi mna kitabu kilichoteremshwa kutoka mbinguni ambacho mnakuta ndani yake kuwa mtiifu ni kama muasi, mkawa mnayasoma hayo mnayoyasema?
Hivyo basi nyinyi ndani ya kitabu hiki mna kila mnachokitamani. Basi hilo nyinyi hamnalo.
Au nyinyi mna ahadi na mapatano ya lazima juu yetu kuwa mtapata mnayoyataka na kuyatamani?
Waulize washirikina, ewe Mtume, «Ni yupi katika wao anayeichukulia hukumu hiyo dhamana na ahadi kwamba atayapata hayo?»
Au wau wana waungu wanaowachukulia dhamana kwa wanayoyasema na kuwasaidia kuyafikia hayo wanayoyataka? Basi na wawalete iwapo wao ni wakweli katika madai yao.
Siku ya Kiyama, mambo yatakuwa magumu na kituko chake kitakuwa kikubwa, na hapo Mwenyezi Mungu Aje ili kutoa uamuzi baina ya viumbe, Afunue muundi Wake usiofanana na kitu chochote. Amesema, rehema ya Mwenyezi Mungu na amani zimshukie, «Atafunua Mola wetu muundi Wake, hapo amsujudie kila mwanamume aliyeamini na mwanamke aliyeamini, na atasalia yule aliyekuwa akisujudu duniani kwa kujionesha na kusikika, aende kusujudu na mgongo wake ugeuke kuwa mfupa mmoja.» Imepokewa na Bukhari na Muslim.
Yatakuwa yameinama macho yao, hawayainui, wamefinikwa na unyonge mkubwa kutokana na adhabu ya Mwenyezi Mungu, na hali wao walikuwa ulimwenguni wakiitwa kuswali na kumumuabudu Mwenyezi Mungu wakiwa na nguvu zao na uwezo wa kufanya hivyo, wakawa hawasujudu kwa kiburi na kujiona wakubwa.
Basi, niache, ewe Mtume, na wale wanaoikanusha hii Qur’ani! Ni juu yangu kuwalipa na kuwatesa. Tutawanyoshea mambo yao kwa kuwapa mali, watoto na neema nyiginezo kwa njia ya kuwavutavuta kwa namna ya wao kutofahamu kuwa hiyo ndiyo njia ya kuwaangamiza.
Na ninawapa muhula na kuurefusha umri wao, wapate kuendelea kufanya dhambi. Hakika vitimbi vyangu kwa watu makafiri ni vya nguvu na vikali.
Au unaomba, ewe Mtume, hawa washirikina ujira wa kidunia kwa kuufikisha ujumbe, hivyo basi wao wakawa wamelazimishwa kubeba mzigo mzito wa gharama?
Au wao wana ujuzi wa ghaibu, wakawa wanaandika kutokana nao kile wanachokiamulia nafsi zao kwamba wao wana cheo bora zaidi kwa Mwenyezi Mungu kuliko wale wenye kumuamini?
Basi vumilia, ewe Mtume, kwa kile Alichokiamua Mola wako na kukipitisha. Na miongoni mwa hivyo ni kuwapa muhula na kuchelewesha ushindi wako kwao. Na usiwe ni kama yule mtu wa chewa, naye ni Yūnus, amani imshukie, alipokasirika na kutokuwa na uvumilivu na watu wake, pindi alipomuita Mola Wake, na huku amejawa na makero, akimuomba Awaharakishie adhabu,
lau si yeye kufikiwa na neema ya Mola Wake kwa kumwafikia kutubia, angalitupwa chini, kutoka tumboni mwa chewa, kwenye ardhi kavu yenye kuangamiza, na hali amefanya jambo la kulaumiwa.
Mola Wake Akamchagua kwa ujumbe Wake, Akamjaalia ni miongoni mwa watu wema waliokuwa wazuri wa nia, matendo na maneno.
Kwa hakika wanakaribia makafiri wanapoisikia Qur’ani kukudhuru kwa jicho la uhasidi kwa kukuchukia, lau si Mwenyezi Mungu kukuokoa na kukuhami, na wanasema kwa matamanio yao kwamba yeye ni Mwendawazimu.
Na haikuwa Qur’ani isipokuwa ni mawaidha na ukumbusho kwa viumbe wote miongoni mwa binadamu na majini.
Icon